Tuesday, October 23, 2012

MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA NA MATISHIO YAKE YA KUKIFUTA CHADEMA KATIKA DAFTARI LAKE.

                            Na  Festo  Mukerebe

Pengine kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu, Watanzania hivi karibuni tulishuhudia mauaji ya mwandishi wa habari za luninga wa Channel Ten, David Mwangosi, huko Nyololo, Mufindi, Iringa. Inasadikiwa kwamba Mwangosi alikuwa amekwenda katika Kijiji cha Nyololo kufuatilia taarifa za kukamatwa kwa mwandishi wa habari wa gazeti la Nipashe, ambaye alikuwa ametiwa mbaroni na jeshi la polisi huko huko Mkoani Iringa.
Mzizi na chanzo cha tukio hilo ni sherehe za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) za uzinduzi wa ofisi ya tawi lake jipya, ambazo chama tawala, C.C.M., kilikerwa kuona jinsi zilivyovutia waandishi wa vyombo mbali mbali vya habari kuziwekea kumbukumbu.
Hukumu ya kifo cha Mwangosi, ilitolewa na askari mmoja wa cheo cha chini katika jeshi la polisi, aliyeamua kumaliza udhia kwa kumlipua kwa bomu Mwangosi sehemu ya tumbo lake. Kitendo hicho kilifanyika baada ya kushirikiana na askari polisi wengine, wasiopungua saba (kwa mujibu wa picha zilizochukuliwa wakati tukio hilo likiwa linaendelea) kumzonga Mwangosi na kudhibiti harakati zake za kuchukua picha za hali halisi ya mambo ilivyokuwa katika eneo lile, huku Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa, Mchael Kamuhanda, akisemekana kuwapo kushuhudia (na kuamuru?) mauaji hayo!
Sio madhumuni yangu kulijadili kwa undani tukio hili, kwani naamini kwamba tayari liko Mahakamani. Isitoshe, tumezoea kuzuiwa kuyajadili matukio kama hayo kwa mantiki na msingi kwamba yamefikishwa Mahakamani. Kila kukicha,  tunaambiwa kuwa kufanya hivyo, ni kinyume kabisa cha matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania!
Kwani ni mara ngapi mwaka huu tumeshuhudia marufuku hii ikitamkwa kwa ukali na msisitizo mkubwa na serikali, hususan Bungeni? Migomo ya Madaktari na Walimu ilizuiliwa kabisa hata kuzungumzwa tu katika vikao vya Bunge la Bajeti, kwa maelezo ya kuwa kwake tayari mbele ya Mahakama. Tumeambiwa mara nyingi kwamba, Mahakama, kama mmoja wa Mihimili yetu ya dola,  si ruhusa kwa Mihimili miwili mingine ya Bunge na Serikali, kuingilia mambo yake!
Shida iliyonisukuma kuandika makala hii, haina uhusiano wa moja kwa moja na mantiki ya kanuni hiyo. Jambo linalosumbua kichwa changu ni kauli na vitisho  vya Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji John Tendwa, kwamba hatasita kukifuta katika Daftari lake, Chama chochote cha siasa, ambacho mkutano wake wa kisiasa utapelekea kutokea kwa mauaji.
Kimsingi, naunga mkono msimamo mkali wa Msajili, kwani matukio ya mauaji katika nchi yetu yameongezeka kwa kasi mnamo miaka ya karibuni; na kwa vyovyote vile, hali hiyo ya upotevu wa uhai wa raia wa nchi hii wasiokuwa na hatia, haiwezi kuendelea kuvumiliwa zaidi.
Wasiwasi wangu ni ubavu wa Msajili kuitekeleza kwa ufanisi na bila upendeleo wowote, azma yake hiyo ya kujitutumua. Hadi sasa, mauaji mengi yamefanywa na jeshi la polisi, likiwa katika harakati za kudhibiti maandamano na mikutano ya Vyama vya Upinzani, hususan CHADEMA na CUF. Binafsi sijawahi kusikia jeshi la polisi likipambana na Chama Tawala, CCM, wakati wa mikutano na maandamano yaliyoandaliwa na Chama hicho.
Nitaikubali shingo upande hoja kwamba Chama Cha Mapinduzi, C.C.M., ni chama chenye maadili na nidhamu ya hali ya juu sana, kiasi kwamba chenyewe kamwe hakivunji au kukiuka kanuni na taratibu za mikutano na maandamano, kama zilivyowekwa na mamlaka husika.
Lakini napata taabu zaidi kuamini nidhamu hiyo, hasa ninapofuatilia mwenendo wa baadhi ya wanasiasa waandamizi wa Chama Cha Mapinduzi, wanapokuwa wakichangia mijadala Bungeni au kuhutubia mikutano ya kampeni za chaguzi ndogo majimboni. Sikusudii hapa kuwataja kwa majina viongozi hao. Lakini Watanzania wengi wana macho na bongo nzuri. Fumbo mfumbie mjinga!
Sambamba na hali hiyo, najiuliza kama atakuwapo mwamuzi asiyefungamana na upande wowote, atakayepitisha hukumu ya haki ya nani  mwenye kutimiza vigezo vyote vya nidhamu inayokubalika kuhusiana na uendeshaji wa mikutano na maandamano yenye ushindani mkali wa kisiasa, kuelekea 2015.
Hivi kweli wanaweza kuwa ni watendaji wateule wa Serikali ya Chama Cha Mapinduzi, sampuli ya Jaji Tendwa? Na kama watendaji hawa wataamua, kwa maslahi ya ajira zao nono, kukibeba Chama cha mrengo wao, na kuvikata ndimi na kauli vyama vyenye upinzani mkubwa kwao, ni nani atasimama kuvisemea na kuvitetea hivyo vyama vya upinzani? Kweli vitakuwa salama? Ah wapi!
Nina hakika kwamba C.C.M. kikiamua kuasisi ghasia  fujo na machafuko katika mikutano na maandamano ya vyama wasivyovipenda, Msajili hatasita kuitekeleza azma yake kwa kukifuta chama husika. Huenda sasa anajenga mazingira ya kufanya hivyo mbele ya safari.
Lakini endapo CHADEMA nacho, kwa mfano, kikianzisha fujo za aina hiyo kwenye mikutano au maandamano ya Chama Cha Mapinduzi, hivi kweli tuamini kwamba Jaji Tendwa  atakuwa na satwa, utashi na ubavu wa kukifuta Chama hicho Tawala katika Daftari lake? Thubutu! Akale wapi?
Ushauri wangu wa bure kwa Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, ni kwamba awe muangalifu na makini sana katika utekelezaji wa matishio yake. Asipofanya hivyo, asishangae kujikuta anapelekea nchi yetu kuingia katika machafuko na vita ya wenyewe kwa wenyewe, kama tulivyoshuhudia katika mataifa mengine ya Afrika, hususan Misri, Libya na Tunisia. Kwa maana mimi sioni jinsi vyama vya upinzani vyente ufuasi mkubwa katika umma wa nchi yetu, vitakavyokuwa tayari kufutiwa usajili wake kirahisi na kwa mbinu za ujanja ujanja; na bado vikubali kukaa kimya mithili ya kondoo anayepelekwa machinjioni. Lazima vitapambana tu. Chonde chonde Msajili wetu, atuepushe na zahma hiyo!  
Lakini lipo jambo jingine linalohusiana na hili, linalonitia mashaka makubwa. Baada ya matukio ya mauaji ya kisiasa yaliyotekelezwa na Jeshi la Polisi huko Morogoro na Iringa mwaka huu, achilia mbali matukio ya mengine kama hayo huko Arusha, Tarime, Songea, Igunga, Aru Meru, n.k., Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, amesikika akimshangaa Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP, Saidi Mwema, kwa kuchelewa kumkamata na kumtia ndani mara moja, Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Wilbrod Slaa.
Kisa nini, ati? Eti Dk. Slaa aliwahi kumtumia Kamanda Mwema ujumbe mfupi wa simu akitahadharisha kuhusu kuibuka na kuenea kwa wimbi hatarishi la mauaji ya kisiasa nchini. Sasa kwa vile mauaji ya mwandishi wa habari Mwangosi, yalitokea siku chache baada ya ujumbe huo, basi Dk. Slaa alikuwa ni injinia mkuu wa mauaji hayo! Na hivyo, alistahili kutiwa kitanzi! Ebo! Hivi kweli Waziri Nchimbi hajawahi kusikia au kuelewa mantiki ya msemo wa wahenga kwamba: “Tarishi hauawi”.
Vinginevyo, Waziri asingaliweza kuyahusisha kirahisi mambo hayo mawili tofauti - mauaji ya Mwangosi na ujumbe wa Dk. Slaa kwa IGP. Mbona Waziri haonyeshi hata dalili tu ya kupepesa kope kwa kuwaona Kamanda Kamuhanda na askari aliyemfumua kwa ukatili wa kutisha mwandishi Mwangosi wakiendelea kupeta mitaani, wakiwa huru kazini mwao, utadhani marehemu Mwangosi hakuwa ‘mtu kitu’. Sijui tutaendelea hadi lini kujiuliza kama askari muuaji alikuwa anatekeleza amri ya Kamanda wake, au aliamua tu kwa ridhaa yake mwenyewe kumpoka uhai mwandishi wa habari. Na tusubiri miezi ijayo taarifa za hizo tume lukuki zilizoundwa na waheshimiwa kutuambia kulikoni!
Kwa mbali, mimi naweza kumuona Waziri Nchimbi akijaribu kulinusuru jeshi lake la polisi, kama sio kujinusuru yeye mwenyewe, akiwa bosi mkuu wa jeshi hilo nchini; lakini  tafakuri ndogo tu inanituma nimuone Waziri akigonga mwamba kwa kishindo katika kadhia hii.
Kwa kuhitimisha makala hii, mimi ningelidhani kwamba wakati ulikuwa unatishia kukipita Chama Cha Mapinduzi, makada wake wababe (kina Mwigulu Nchemba, Livingstone Lusinde, John Tendwa na wengineo kama Ismael Aden Rage mwenye kudiriki kutembea na silaha ya moto kiunoni hadharani). Kama kweli wanakitakia maisha mema Chama chao, CCM,  baada ya 2015, wangelishaurika kurudi haraka kwenye drawing boards za mikakati.
Ni kwa manufaa ya makada na washabiki wa Chama cha Mapinduzi kutambua kwamba shida kuu ya Watanzania, ni maisha bora ya kweli. Haijalishi hata wakiletewa na shetani maisha hayo

No comments:

Post a Comment