Tuesday, October 23, 2012

MOVEMENT FOR CHANGE, M4C, VUA GAMBA VAA GWANDA, MABADILIKO MANNE CHANYA, OPERESHENI SANGARA; VISION FOR CHANGE, MCHAKAMCHAKA HADI 2015;  MISSION FOR CHANGE;  ARI ZAIDI, NGUVU ZAIDI NA KASI ZAIDI, MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA;… WATANZANIA TUNA KAZI KUELEKEA 2015.

                                    Na  Festo Mukerebe

Mwaka 1960, Waziri Mkuu wa Uingereza (Macmillan?), alizungumzia kile alichokielezea kama ‘Kimbunga cha Mabadiliko Barani Afrika’ (“The wind of change”, alisema “is blowing across Africa”. Makoloni kama India yalikuwa tayari yamefanikiwa kujipatia uhuru (1948); na mengine, yakiwemo ya Afrika, yalikuwa hayako tayari kuendelea kutawaliwa na kudhibitiwa na mataifa ya Ulaya. Kuanzia wakati huo, Mabadiliko makubwa yalikuwa hayawezi kuepukika tena.
Mwaka 2008, mgombea urais wa Marekani kwa tiketi ya Chama cha Democrat, mweusi Barak Obama, aliitumia kwa mafanikio makubwa Kauli-mbiu (au slogan) ya Mabadiliko,Change, kuingia Ikulu, huku akiwahamasisha Wamarekani kuamini katika uwezo wake wa kuinasua nchi hiyo kutokana na madhila mbalimbali waliyoletewa na utawala ‘mbaya’ wa Rais wa tiketi ya chama cha Republican aliyemtangulia, George Bush. “Yes we can”, aliwahakikishia na kuwashawishi wapiga kura hadi kuamua kumsabilia uongozi wa taifa hilo kubwa ulimwenguni. Baada ya karne nyingi za udhalimu na ukandamizaji, enzi za dharau kwa mtu mweusi, zilikuwa hatimaye zimefikia tamati na kutokomea.
Miaka ya karibuni, Tanzania imeshuhudia kimbunga cha Kauli-mbiu za Mabadiliko katika medani za siasa za chaguzi za vyama vingi . Tulianza kuzisikia Kauli-mbiu hizi wakati wa kampeni za Urais za kipindi cha kwanza cha Awamu ya Nne, ambapo Chama Cha Mapinduzi (C.C.M.) kiliibuka na “Ari Mpya, Nguvu Mpya na Kasi Mpya” (ANGUKA) na “Maisha Bora kwa Kila Mtanzania”.
Kutokana na ufanisi kiduchu uliopatikana katika miaka mitano ya kipindi cha kwanza cha utawala wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, kauli-mbinu hizo hizo zilifanyiwa  ukarabati kusudi wananchi waendelee kuamini  kwamba C.C.M bado kinaweza!. Kauli-mbiu ya “ANGUKA”, kwa mfano, ikakolezwa kwa nyongeza ya neno ‘ZAIDI’- “ Ari Zaidi, Nguvu Zaidi na Kasi Zaidi”. Tatizo la C.C.M. hapa ni kutambua, bila kuwa na la maana la kufanya, kwamba mahasimu wake wanakisuta kwa kukiita “Chama cha ANGUKA ZAIDI”!
Siku za hivi karibuni, vyama vingine vya siasa navyo vimezinduka na kuona kuwa haiba zake hazikamiliki bila kubuni na kusanifu kauli-mbiu zenye ushindani katika soko la mvuto na haiba kwa Watanzania wanaoandaliwa kwa kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), wamekuja na “Vuguvugu la Mabadiliko”, maarufu kama “Movement for Change”. Wakati mwingine, kauli-mbiu hii inatiwa kionjo kwa kuitwa “Mabadiliko Manne Chanya” au “M4C”.
Chama cha Wananchi (CUF), hakikukubali kuachwa nyuma katika mkumbo huu mpya wa Mabadiliko. Kichekwe? Chenyewe kimeibuka na Kauli-mbiu za “Vision for Change” na “Mchakamchaka Hadi 2015”. Sina hakika zilikoishia Kauli-mbiu zake za awali za “Ngangari” na “Haki Sawa Kwa Wote”.
Nacho SAU kinasemekana kuwa mbioni, si muda mrefu ujao, kuzindua kauli-mbiu ya “Mission for Change”.
Kwa rekodi iliyofikiwa hadi sasa, hapana shaka kwamba orodha ya Kauli-mbiu hizi itakuwa ndefu zaidi kadiri siku zinavyokatika kuelekea kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mkuu, mwaka 2015.
Binafsi, sina tatizo na harakati hizi za ushindanishi wa Kauli-mbiu za vyama katika mbio za kujinadi na kujigamba mbele ya Watanzania, ambao muda si Miaka mingi  ijayo, watakuwa wakimiliki tena nguvu ya turufu (veto) kuhusu mustakabali wa utawala wa nchi yetu, fursa ambayo huwajia mara moja katika kila miaka mitano, kwa mujibu wa Katiba ya nchi yetu.
Shida yangu ni mantiki ya msemo wa Kiswahili usemao: “ Miluzi mingi huwapoteza mbwa”. Maana sina hakika na uwezo wa Watanzania tulio wengi kuzipembua na kuzipambanua kwa “ukweli na uwazi” kauli - mbiu zote hizi, achilia mbali na kuzihusisha na hali halisi ya utendaji wa vyama vyetu, ili tuweze hatimaye kufanya maamuzi chanya, hekima na busara (informed decisions), come 2015, for our own fate and betterment. Mungu Ibariki Tanzania.

No comments:

Post a Comment