VYAMA VYA UPINZANI VIJIEPUSHE KUSHEREHEKEA USHINDI
USIOPATIKANA BADO
Na Festo Mukerebe
Mwandishi mmoja wa Afrika ya Magharibi, Ayi Kwei Armah, alikiita kitabu chake cha kifalsafa: The Beautiful Ones Are Not Yet Born. Kadiri ya mantiki ya kitabu hicho na mwenendo wa matukio ya enzi zetu hizi, ni wazi kwamba, Mwandishi huyo hakukosea hata chembe.
Mimi sikuwahi kukipenda Chama cha Mapinduzi, japo katika miaka yake ya awali, nilikuwa na Kadi ya uanachama. Hata hivyo, sijawahi kumbaini kiongozi bora kama muasisi wa chama hicho, Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius K. Nyerere.
Kama ningalibanwa kuthibitisha ukweli wa mapenzi yangu kwa Mwalimu, wala nisingalihitaji kwenda mbali sana. Watu walio karibu na mimi watakuwa wamebaini siku nyingi kwamba ni nadra sana niwapo mapumzikoni nyumbani kwangu siku ipite bila kufungulia redio yangu kukisikiliza kipindi cha Wosia wa Baba, ambacho hudhaminiwa na Shirika la Taifa la Mbuga za Wanyama nchini (TANAPA) na kurushwa na Kituo cha Televisheni cha TBC kati ya saa 2.15- 2.30 usiku, isipokuwa siku za Jumapili. Nakihusudu kupindukia kipindi hicho kwa sababu ya hotuba zake zisizochosha wala kuchusha.
Aidha, kwa miaka mingi pia, asilimia kubwa ya vitabu nilivyojitahidi kununua kwa ajili ya maktaba yangu ya nyumbani (home library), ni vile vinavyohusiana moja kwa moja na kazi za Mwalimu kitaifa na kimataifa, baada ya uhuru na hata baada ya kung’atuka kwake uongozi wa chama na serikali.
Ni rai yangu ya dhati kwamba kama ipo tunu kubwa ambayo Watanzania tutakujajuta kuikosa katika maisha yetu ya sasa na ya vizazi vingi vijavyo, tunu hiyo ni hotuba zake, zile rasmi na hata zile ambazo Waingereza huziita impromptu, kwa maana ya zile zisizoandaliwa awali.
Ama kweli, Mwalimu alikuwa amejaliwa kipaji kisichomithilika cha kuzungumza na kuhutubia. Ningalikuwa na mamlaka tosha, ningalielekeza kipindi cha Wosia wa Baba sio tu kirushwe kila siku , bali kipewe muda usiopungua saa nzima. Robo saa ya sasa haikidhi hamu ya baadhi yetu ambao tumetokea kuwa na mzio chanya (positive addiction) na hotuba zenye mvuto mkubwa za gwiji hilo la siasa duniani.
Hivi ni kwa kiasi gani sisi Watanzania tunavihitaji vipindi vya muziki wanaouita wa ‘kizazi kipya’ na vingine kama ‘Bango’(matukio ya watu binafsi) na ‘Chereko’ (nadhiri za uongo na viapo vya kudanganyana ‘wapendanao’) ambavyo vinatufanya watu wazima tuonekane mazezeta mbele ya TV zetu, tukitumia muda wetu mwingi kukodolea program zisizokuwa na tija kwa maisha yetu?
Mwanzoni mwa makala hii, nimesema kwamba sijapata kukipenda Chama Cha Mapinduzi, hata kama ndicho chama alichopata kukiongoza Mwalimu. Nilimpenda Mwalimu bila kukipenda CCM. Hiyo ni kwa sababu kwa kila hatua, mimi huwa naiuliza nafsi yangu kama C.C.M. na serikali yake kweli ilikuwa inakidhi matakwa na utashi wangu katika maisha. Nyakati za Uchaguzi Mkuu, mimi hutazamia kila Mtanzania aihoji nafsi yake swali hilo kabla hajaamua kukipigia kura chama hicho. Sina hakika kama huwa wanafanya hivyo!
Hivi karibuni, niliandika makala moja kueleza kwa nini nilikua sijisikii kushiriki zoezi la Sensa ya Idadi ya Watu na Makazi ya mwaka huu, 2012. Ili nisihusishwe na Waislamu wenye imani kali, nililazimika kueleza sababu zangu za kughairi zoezi lile (japo wakati wa Sensa yenyewe ulipowadia, nilijikongoja kushiriki kikamilifu). Moja ya sababu hizo, ilikuwa ni kushindwa kuona matunda ya kushiriki kwangu katika Sensa nyingi zilizotangulia (1957, 1967, 1978 na 2002).
Nilihoji kwa nini njia ya miguu niliyotembea peku mwaka 1961 (zaidi ya miaka 50 iliyopita) kwenda kuanza maisha ya shule, imeendelea kubaki ile ile hadi leo; mbona shule yenyewe (Kashumbililo Shule ya Msingi) haijabadilika sana hadi leo (licha ya kupandishwa hadhi kutoka darasa 4 hadi darasa la 7); mbona zahanati ya Kata yetu, Izigo, niliyoshiriki kwaya ya shule yangu kuifungua mwaka 1964, haijabadilika hadi sasa (kwa maana ya miundo-mbinu na ubora wa huduma zake, n.k.? Sasa nishiriki Sensa nyingine ili iweje?
Najikuta nikishindwa kukipambanua Chama Cha Mapinduzi na mapungufu yote hayo (na mengine mengi ambayo nafasi ya makala hii haitoshi kuyataja). Kwangu mimi, mapungufu hayo ni kielelezo tosha cha kushindwa kwa Chama hicho kumuenzi ipasavyo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere. Hata kushindwa kwa serikali kukitengea muda wa kuridhisha kipindi cha Wosia wa Baba kuwa hewani kupitia chaneli yake ya Taifa, TBC, ni udhaifu mwingine ulio dhahiri.
Pengine jambo rahisi kama hilo linashindikana kufanyiwa kazi kwa sababu Hotuba zenyewe za Mwalimu kwa mantiki yake zinausuta uongozi na mwenendo mzima wa Chama hicho, haijalishi kwamba ni yeye mwenyewe aliyekiasisi na kukipa uhai wake. Kwani si aliwahi kukiri kwamba Chama hicho hakikuwa mama yake mzazi kiasi kwamba asiweze kufarakana nacho, ikibidi kufanya hivyo?
Watu wengi wenye uelekeo kama wa kwangu, mintarafu siasa za Tanzania, wananiaminisha kwamba wanatazamia mwaka 2015 tutashuhudia mwisho wa Chama Cha Mapinduzi kama Chama Tawala katika siasa za Tanzania. Na mimi binafsi ningalitamani iwe hivyo. Lakini kwa bahati mbaya, wishes are not horses.
Ni kweli kwamba Chama Cha Mapinduzi hakitakuwa chama tawala cha kwanza barani Afrika kupoteza usukani. Yaliwahi kukitokea UNIP cha Zambia, cha KANU nchini Kenya na cha MCP nchini Malawi. Aidha, bado tunafuatilia mambo yanayoendelea kutokea kwa vyama tawala vya nchi zilizofanikiwa kuung’oa utawala wa nchi zao kasikazini mwa Bara la Afrika, ikiwa ni pamoja na Algeria, Tunisia, Misiri na Libya. Kwa hiyo, ni kweli kwamba mabadiliko kama hayo ni mambo yanayowezekana kabisa kutokea kwa chama kingine chochote, haijalishi ni kikongwe kiasi gani.
Lakini yatakuwa ni makosa na kujidanganya kufikiri kwamba jambo kama hilo litakuwa ni rahisi kutokea kwa Chama Cha Mapinduzi. Kwa nini? Kwa sababu vyama ambavyo vimeendelea kuwa madarakani barani Afrika, vilikwishashituka na kukaa chonjo, tofautina kina UNIP vilivyoshitukizwa na mabadiliko. Kwa vyovyote vile, vyama vikongwe madarakani kama Chama Cha Mapinduzi, ZANU- PF, haviko tayari kufuata nyayo ya vyama tangulizi vya UNIP, KANU, MCP na vinginevyo vilivyoanguka mweleka wa mende. Vyama hivi vitang’ang’ania madarakani kama papasi afanyavyo juu ya kiwele cha ng’ombe, liwalo na liwe!.
Kwetu Tanzania, hali inaweza hata kuwa ngumu zaidi, kwani wapo baadhi ya Watanzania ambao hadi sasa hawajafanikiwa kukipambanua Chama Cha Mapinduzi na Mwalimu Nyerere pamoja na Sera yake ya Ujamaa na Kujitegemea, siasa iliyotukuka nchini kwa miongo kadhaa kabla ya kifo chake mwaka 1999. Mifano michache yaweza kutolewa kulithibitisha jambo hili.
Wakati Tanzania ilipolazimika kutohoa mfumo wa vyama vingi, Mwalimu Nyerere, kwa upeo wake mkubwa, aliwapa changamoto wahafidhina wa siasa za chama kimoja ambao hawakuwa tayari kwa mabadiliko, kujizatiti kwa sababu za miaka ya Tisini (na sio zile za miaka ya Sitini zilizopitwa na wakati), la sivyo wakubali kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa.
Kwa vile wahafidhina hawakuwa na sababu zenye mantiki wala uwezo wa kukabiliana na changamoto ya Mwalimu Nyerere, walijaribu kuibua hisia za vitisho na hofu kwamba vyama vingi vingezua mitafaruku katika jamii ambayo ingaliitumbukiza nchi katika lindi la mauaji ya kimbari, kama yale ya nchi jirani za Ruanda na Burundi. Kina mama na wazee waliogopeshwa sana kwa sinema zilizoonyesha wanawake wajawazito wakitumbuliwa matumbo yao na mimba zao kunyotolewa kwa ukatili na mateso ya kinyama!
Ni katika mazingira hayo kwa jumla, ndimo hatimaye mfumo wa siasa ya vyama vingi ulijikuta unazaliwa nchini Tanzania. Na kwa bahati mbaya, kizazi kilichotishwa na kutishika na wahafidhina waliopinga kuanzishwa kwa mfumo huo, bado kinadumu na huenda sumu ya mawazo yake, itachukua miaka mingi zaidi kufifia na kutoweka kabisa.
Niliwahi kushuhudia mara kadhaa kijiji cha nyumbani kwetu (jina la kijiji kapuni) kikitisika kwa mihemko ya kusherehekea ushindi wa Diwani wa Kata aliyepita kwa tiketi ya Chama Chama Mapinduzi. Mzee yule (jina linahifadhiwa), alikuwa tayari amedumu katika wadhifa ule kwa zaidi ya mihula mitatu, yenye jumla ya miaka isiyopungua thelathini! Baadhi yetu tuliendelea kujiuliza ni kwa rekodi gani mzee yule alikuwa ameendelea kupigiwa kura za ushindi katika Kata yetu!
Katika dadisi zangu binafsi, hatimaye nilifanikiwa kugundua kwa nini. Wazee wengi wa vijiji vya kwetu na, hasa kina mama, walitegemea zaidi mauzo ya gongo (enkonyagi) kwa maisha yao ya kila siku. Lakini kwa vile kwa sheria za nchi yetu pombe hiyo ni haramu, shughuli hiyo iliwatia hofu ya kushukiwa na mkono wa nguvu za dola.
Kwa bahati, Diwani ‘wao’ alielekea kuwakingia kifua dhidi ya hatua za kisheria pale askari polisi au mgambo walipovamia vijijini, kwa taarifa au vinginevyo. Ni kwa msingi huo sasa, wazee walikuwa hawaambiliki wakati wa kupiga kura, kwani kiongozi huyo alikuwa ni tumaini na mtetezi wao wakati wa misako ya gongo, kodi na uhalifu mwingine mdogo mdogo vijijini.
Katika dadisi zangu nyakati za uchaguzi wa vyama vingi, nimewahi kuwasikia kina mama wakihoji ni chama gani zaidi ya CCM ambacho wangalikipigia kura. Mmoja wao (jina kapuni) aliuliza: “ Hivi kweli bila CCM watu tunaweza kuishi?”
Ndiyo maana mimi binafsi sishangai tena kumuona kiongozi wa CCM akidumu katika nafasi ya uongozi kwa miaka chungu nzima hata kama hana jambo la maana la kuonyesha kama matunda ya uongozi wake. Kwani nimegundua kwamba kiongozi anayewania kuchaguliwa tena na tena sio lazima apimwe kwa misingi ya mambo chanya aliyowahi kufanikisha utekelezaji wake mnamo vipindi vya awali vya uongozi wake. Wahalifu watatu au wanne aliowasaidia wasikabiliane na mkono wa nguvu ya dola, ni mtaji wa kutosha kumuwezesha kujikusanyia kura za ushindi katika kijiji kimoja au kingine.
Nimewahi kufadhaishwa sana na matokeo ya kinyang’anyiro cha uchaguzi katika kijiji kimoja cha kwetu (jina linahifadhiwa) ambapo askari polisi mmoja mstaafu (jina kapuni) alikuwa anagombea fursa ya uongozi kwa tiketi ya chama cha upinzani. Wengi wetu ambao tuliwahi kuwa karibu na mstaafu huyo na kutambua upeo na uwezo wake, tulimuona kama lulu ambayo kijiji chetu kilikuwa kimejaliwa kuipata katika safu ya uongozi kwa ngazi hiyo.
Hatukuamini taarifa zilizotufikia baadaye kwamba askari polisi mstaafu yule alikuwa amegaragazwa vibaya na kijana (asiyekuwa na jina kisiasa kijijini) aliyegombea kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi. Kisa? Mosi, eti askari polisi wana roho mbaya (‘ebipolisi bigil’ omwoyo gubi’); na pili, vyovyote vile mtu kama huyu angalitokea kuwa kipingamizi kikubwa kwa shughuli zao za kiuhalifu zisisizoendana na utawala wa sheria.
Kwa nini ninayaandika yote haya? Nayaandika kuwataadharisha viongozi na wakereketwa wa vyama vya Upinzani ambao wanaelekea kukumbwa na kiwewe cha imani kwamba 2015 ni mwaka wa Watanzania kushuhudia kaburi la Chama Cha Mapinduzi. Pamoja na baadhi yetu kufurahika na mtazamo huo, bado mimi naziona hizo kama ndoto za Alinacha! Na kamwe sipendi kufananishwa na mbwa mwitu ambaye alimnyemelea binadamu kwa masafa marefu hadi mlangoni kwake kwa matarajio ya kuokota mikono yake aliyoiona iko mbioni kukongoroka na kudondoka chini wakati wowote!
Hivi karibuni, wakati wa uchaguzi wa ndani wa Chama Cha Mapinduzi, Mwenyekiti wa chama hicho tawala, Jakaya Mrisho Kikwete, alisikika akiwasuta na kuwakebehi Watanzania wasiokitakia CCM mema na uhai baada ya Uchaguzi Mkuu 2015, kwamba watakufa wao wenyewe na kukiacha chama hicho kikiendelea kudunda kwenye uongozi wa nchi kwa miaka mingi zaidi ijayo. Kwa hakika siifurahii kauli hiyo, lakini sipendi kuipuuza hata kidogo; kwa sababu nawafahamu vizuri Watanzania. Naona na Kikwete anawafahamu vilivyo watu wake.
Kwa baadhi yetu, ni jambo lililo dhahiri kwamba Chama Cha Mapinduzi kimejifikisha katika hatua ya udhaifu mkubwa tangu kuasisiwa kwake miaka 60 iliyopita. Na kwa vyovyote vile, hakuna namna ya kulinganisha nguvu zake leo na wakati wa miaka ya themanini, kwa mfano.
Tuchukue tukio la ‘kuchafuka kwa hali ya hewa’ kama kielelezo na kigezo cha tofauti za Chama hiki kwa nyakati hizo. Mwaka 1984, Chama Cha Mapinduzi, chini ya uongozi madhubuti wa Mwalimu Nyerere, kilidiriki kumtimua uongozi Makamu wa Kwanza wa Rais, Alhaj Aboud Jumbe. Kiongozi huyo aliondoka kwenda Dodoma akiwa ni mtu wa pili tu nchini nyuma ya Nyerere kwa madaraka, nguvu na mamlaka, lakini alirejea Zanzibar akiwa raia wa kawaida tu. Na wala hatukumsikia Rais Nyerere kumshikia bastola au chombo chochote cha moto kama tunavyoshuhudia viongozi ndani ya utawala wa CCM (kina Ismael Aden Rage, Kigwangala, n.k.) wakifanyiana hivi leo. Misimamo ya kisiasa ya Mwalimu Nyerere ilikuwa ni makombora ya nyuklia ya kung’oa na kusambaratisha milima.
Miaka miwili iliyopita, Chama Cha Mapinduzi kilitikisika vibaya kutokana na ufisadi mkubwa uliodhihirika ndani ya uongozi wake na kutishia kuisambaratisha kabisa haiba yake machoni mwa Watanzania.
Kutokana na uchunguzi wake, Chama Cha Mapinduzi kilibaini na kukiri kwamba angalau vigogo wake watatu walikuwa vinara wa ufisadi ule hatarishi: Waziri Mkuu wa Zamani aliyejiuzuru kwa kashfa ya Rushwa ya Richmond, Mwanasheria Mkuu wa Serikali wa Zamani, Andrew Chenge na Mbunge wa Igunga aliyepata kuwa Mweka Hazina wa Chama Cha Mapinduzi, Rostam Aziz. Hatukupata kushuhudia vishindo vya kutimuana vya enzi za Mwalimu.
Badala yake, tulitangaziwa mradi wa Chama wa kuwatokomeza mafisadi wale, kama mkakati wake wa kujisafisha mbele ya umma. Lakinini kitu gani kimetokea hadi leo?
Ukiondoa Rostam Aziz aliyetangaza kushindwa kuendesha ‘siasa za maji taka’ na hivyo kuamua kwa hiari yake kujiuzulu nafasi zake zote za uongozi, tumewashuhudia wenzake wakizidi kuchanja mbuga kwa kuendelea kushikilia nyadhifa zao zote, kama sio kuongezewa nyingine nyingi tu, kama vile hakuna jambo lolote lililopata kutokea katika maisha yao ya kisiasa!
Lugha inayotawala anga za siasa nchini mwetu hivi sasa ni kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mkuu mwaka 2015. Haimshangazi mtu yeyote kusikia kigogo mkuu wa kashfa za Richmond akitajwa kuongoza mbio za kuwania Urais wa Tanzania katika Uchaguzi huo. Nina hakika kwamba kigogo huyo anaingia katika kinyang’anyiro hicho kwa matumaini ya kuibuka mshindi. Nami nitakuwa Mtanzania wa mwisho kushangaa kumuona mtu huyo anaibuka na Urais wa nchi yetu! Kwa nini? Kwa sababu ninawafahamu Watanzania, ambao kura zao ndiyo nyenzo itakayomuinua kwenye kiti cha enzi cha Ikulu miaka hii michache ijayo. Mbona kapeta katika kinyang’anyiro cha uchaguzi uliopita mwaka huu wa Halmashauri Kuu ya Taifa?
Ndiyo maana kila nikimkumbuka Mzee Aboud Jumbe na Rostam Aziz, nashindwa kuelewa ni nini wanakiwaza popote walipo! Ilikuwaje wakakubali kusalimu amri kwa urahisi namna ile wakati ushindi wao ulikuwa mbioni unakuja? Labda isemwavyo ni kweli kuwa unapokaribia kukata tamaa, ndipo ukombozi wako unapokuwa kona ya mwisho kutua mbele yako!
Ninapenda kuhitimisha kwa kuwaasa wapenda mageuzi wa Tanzania kujiepusha na kiwewe cha matumaini bandia ya kifo cha Chama Cha Mapinduzi na matarajio yao ya kunyakua madaraka katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2015. Hii sio Zambia wala Kenya ambako vyama vya UNIP na KANU vilikubali kupigwa teke kwa urahisi, kama ilivyowatokea Mzee Aboud Jumbe na Rostam Aziz wetu.
Yafaa wanamageuzi wa Tanzania wakatambua kwamba wakati wa kusherehekea mabadiliko nchini mwetu bado uko mbali sana. Na si ajabu kuwa Mwandishi wa vitabu wa Afrika Magharibi, Ayi Kwei Armah, alikuwa anatuandikia sisi Watanzania, alipokiita kitabu chake: The Beautiful Ones Are Not Yet Born.